Windows

Dkt. Mwanjelwa awataka waajiri kuzingatia sheria


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Mary Mwanjelwa amewataka waajiri nchini kuhakikisha wanazingatia Sheria, Kanuni na Taratibu wanapowasilisha taarifa za kiutumishi ili kuepuka malalamiko yanahusu stahili mbalimbali za kiutumishi.

Dkt. Mwanjelwa ametoa maagizo hayo alipokuwa akizungumza na Watumishi wa Umma mkoani Kagera wakati wa ziara yake ya kikazi yenye lengo la kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF na kuzungumza na Watumishi wa Umma mkoani humo kuhimiza uwajibikaji.

Dkt. Mwanjelwa amesema zoezi la kusafisha taarifa za watumishi limeibua kero kwa baadhi ya watumishi kutokana na waajiri kutozingatia maadili wanapowasilisha taarifa za kiutumishi.

“Awali baadhi ya waajiri waliwasilisha taarifa za watumishi zisizo sahihi hali iliyosababisha baadhi ya watumishi hao kupewa stahili ambazo si halali na matokeo yake wakati wa zoezi la kusafisha taarifa wamekuwa wakibainika kutostahili na hatimaye watumishi hao kuona kama wameonewa,” Dkt. Mwanjelwa amesisitiza.

Ameongeza kuwa, mtumishi wa umma anakamilika kwa kuwa na tabia njema, nidhamu ya kazi, mwenendo mzuri, weledi na ubunifu, hivyo ni vema kila mtumishi akazingatia hilo ili awe na manufaa kwa umma na tija kiutendaji.

Dkt. Mwanjelwa amesema kuwa, Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga kuhakikisha utumishi wa umma unakaa sawa, kama mtumishi anapaswa kupata haki yake, atapata na kama hastahili aachwe badala ya kupendelewa,” Dkt. Mwanjelwa amesisitiza.

Dkt. Mwanjelwa yuko mkoani Kagera katika ziara ya kikazi kukagua utekelezaji wa shughuli za TASAF na kuhimiza uwajibikaji kwa Watumishi wa Umma katika Halmashauri zote za mkoa huo.

Post a Comment

0 Comments