

LIGI Daraja la kwanza inaendelea kushika kasi na tunashuhudia ushindani ulivyo kwa kila timu kuweka nia ya kupata matokeo ili kupanda daraja na kushiriki Ligi Kuu Bara.
Kuna mengi ambayo yanaendelea kutokana na wengi kuiona kama ligi ya kawaida licha ya uzito wake ambao upo kwani vipaji vingi vinapatikana huko na wachezaji wanajituma.
Mbali na vipaji kupatikana ni sehemu ambayo inahusika kupandisha timu daraja ambayo itapanda na kushiriki Ligi Kuu Bara hivyo ni kitu kikubwa kinaandaliwa.
Kinachohitajika katika kusimamia ni umakini ili kupata timu bora yenye uwezo wa kuhimili mikikimikiki itakapopata nafasi ya kushiriki Ligi Kuu Bara.
Lawama za timu nyingi na wachezaji wanazielekeza kwa waamuzi wanaamini wanashindwa kufuata sheria za mpira hili ni jambo ambalo linahitaji kutazamwa kwa jicho la kipekee.
Ushindani mkubwa kwa kila timu shiriki inamaanisha morali kwa wachezaji ipo juu na benchi la ufundi linafanya kazi yake ipasavyo kupata matokeo hicho ndicho kinachotakiwa.
Kila timu ina nafasi ya kupata matokeo katika ligi, sasa waamuzi mnapaswa muwe makini katika kusimamia haki kwa wachezaji pamoja na timu ili kuepusha makelele kwa viongozi.
Wahusika wa michezo ikiwa ni pamoja na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) itazame namna bora ya kuyafanya mashindano haya itapendeza kama yataonyeshwa moja kwa moja ili kuongeza umakini.
Kwa namna moja ama nyingine itaongeza zaidi umakini kwa waamuzi pamoja na kutoa fursa ya vipaji vyao kuonekana mbali zaidi.
Wachezaji mkiwa uwanjani kazi yenu kutafuta matokeo kwa hali na mali ili mfikie ndoto zenu kwa wakati muafaka.
Onyesheni ushindani ili iwe rahisi kupata matokeo kwenu na inawezekana kupata matokeo uwanjani endapo mtacheza mkiwa ni timu itakuwa rahisi kupata matokeo kwenu.
Tukirejea kwenye michuanao ya kimataifa, wawakilishi wetu Simba tumeshuhudia wakipoteza mchezo wao wa pili katika hatua ya makundi.
Ni matokeo ambayo yanaumiza na hayaleti tija kwa afya ya soka letu, lakini kinachotakiwa kwa sasa ni kufuta makosa ambayo mmeyafanya na kutafuta njia ya kutoka.
Kwenye ulimwengu wa soka mengi yanatokea kikubwa ambacho kwa sasa inabidi kifanyiwe kazi ndani ya Simba ni uongozi kukaa na benchi la ufundi pamoja na wachezji wazungumze.
Kupitia vikao vyao itawasaidia kujua wapi walipokwama na kuanza upya, kazi kubwa iwe kuwajenga kisaikolojia wachezaji warejee kwenye ubora ambao wamekuwa wakionyesha mechi kadhaa zilizopita.
Kundi D ambalo Simba ipo bado hakuna aliyejihakikishia safari ya kufika hatua ya robo fainali ni suala la wakati na matokeo uwanjani kuamua nani ni nani.
Wachezaji mna kazi kubwa ya kuonyesha utofauti wenu mkiwa kwenye mashindano ya kimataifa na kuonesha kwamba mnahitaji kushinda licha ya ushindani mnaokutana nao.
Kwa hapo mlipofikia bado hesabu zinawalinda kutokana na kundi kubaki wazi hasa kulingana na matokeo kwa mechi hizi za mwanzo ambazo zinaleta picha ya kule ambako mnaelekea.
Mmerejea sasa hesabu zenu ziwe mbele zaidi msisahau kuomba radhi kwa mashabiki wenu hasa kwa kitendo mlichokifanya kwani ni maumivu juu ya maumivu, na kuomba kwenu radhi si kwa maneno bali kwa matendo.
Wachezaji onyesheni nia na ari ya kutafuta matokeo katika michezo yenu inayofuata hasa ukizingatia mnakabiliwa na mechi za kimataifa na pia mnapaswa mcheze ligi, muhimu kujipanga.



0 Comments