Genk, Ubelgiji. Timu ya KRC Genk, anayoichezea nahodha wa timu ya taifa la Tanzania ‘Taifa Stars’ , Mbwana Samatta wametangazwa kuwa mabingwa wapya wa Ligi Kuu Ubelgiji ambayo ni maarufu kama Jupiler Pro.
KRC Genk wametangazwa kuwa mabingwa wa Jupiler Pro bada ya kutoka sare ugenini hapo jana ya bao 1-1 na Anderlecht huku wapinzani wao, Club Brugge wakipoteza kwa mabao 2-0 mbele ya Standard Liège.
Matokeo hayo yanamaana kwamba chama la Samatta pamoja na kuwa wamesaliwa na mchezo mmoja kwenye Ligi ndogo yani Play Off kabla ya msimu huu wa 2018/19 kumalizika, wamefikisha idadi ya pointi ambazo hakuna timu inayoweza kuzifikia.
Sare ya bao 1-1 ambayo Genk wametoka usiku wa jana, wamefikisha jumla ya pointi 51 huku wapinzani wao, Club Brugge wakisaliwa na alama zao, 47 kwenye nafasi ya pili.
Sherehe za kuusheherekea ubingwa huo kwa mujibu wa ratiba iliyowekwa kwenye mtandao rasmi wa klabu hiyo zilianza jana, Ijumaa kwa kuzunguka mji wao wa Genk, wakiwa kwenye bus maalumu ambao litakuwa wazi.
Hivyo mashabiki wa wadau mbalimbali wa KRC Genk walipata nafasi ya kuwaona nyota wao, akiwemo Samatta ambao wameifanya timu hiyo kutwaa ubingwa wa nne tangu kuanzishwa kwake, 1988.
Katika mashindano yote msimu huu, Samatta ameifungia Genk jumla ya mabao 32, yakiwemo 23 kwenye Ligi na tisa kwenye Europa Ligi.
Kilichobaki kwa Samatta ni kupigania kiatu cha ufungaji bora wa Ligi Kuu nchini humo ambapo amezidiwa mabao mawili na Mtunisia, Hamdi Harbaoui wa Zulte Waregem mwenye mabao 25.
Samatta mwenye mabao 23 anatakiwa kufunga sio chini ya mabao matatu kwenye mchezo wa mwisho wa msimu dhidi ya Standard Liège huku akimuombea mabaya Harbaoui ili aweze kutwaa kiatu cha dhahabu nchini humo.
0 Comments