Windows

Waziri alaani Vitendo vya udhalilishaji


WAZIRI wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto, Maudline Castico, amelaani kitendo cha udhalilishaji wa kijinsia na mauaji ya msichana mwenye umri wa miaka 19, kilichotokea usiku wa Januari 11, katika mtaa wa Uholanzi, Wilaya ya Magharibi ‘B’ Unguja.

Akifariji familia ya marehemu , Castico alisema vitendo hivyo ni vya kinyama na kikatili na jamii inapaswa kuungana kupambana navyo.

Alisema vijana wanapaswa kujielewa namna ya kutumia nguvu zao katika kazi za halali na sio kuwabaka, kulawiti na kuwaua wanawake na watoto wasio na hatia, vitendo hivyo vinaiweka Zanzibar katika sura mbaya katika macho ya jamii ya kimataifa.

“Sijui tunakwenda wapi na jamii hii itakuaje iwapo mambo haya yataendelea, kila siku wanajaribu kubuni mbinu tofauti za udhalilishaji na sasa yamekuwa ni mauaji ambayo wanafanyiwa wanawake wazee na watoto wasio na makosa yoyote,” alisema.

Alisema wanawake ndio wazazi, walezi na watunzaji wa familia lakini wanahujumiwa kwa kila aina, hivyo mshikamano wa malezi ni muhimu ili kupata vijana bora wa baadae.

“Kwa nini haya mambo yanajirejea, lazima masheha, wazee wa mitaa na waratibu muangalie kwa namna gani mtaweka ulinzi shirikishi na yeyote atakayeoneka anatembea usiku mkubwa mumuhoji na ikiwezekana achukuliwe hatua,” alisema.

Alisema amani na utulivu ndio msingi wa maendeleo hivyo wananchi waungane kuhakikisha hali hiyo inaendelea.

Baadae Castico akiambatana na Naibu wake, Shadia Mohammed, Naibu Katibu Mkuu, Mwajuma Majid na Mkurugenzi Wanawake na Watoto, Nasima Haji Chum, walifika kijiji cha Mangapwani kumuangalia   mtoto wa kike ambaye ni kiziwi aliyebakwa  hivi karibuni.



Post a Comment

0 Comments